RAIS RUTO APONGEZWA KWALE HUKU ALI HASSAN JOHO NA SALIM MVURYA WAKITAKIWA KUEKA KANDO TOFAUTI ZA KISIASA.
Taarifa yake : Caroline Katana
Wakaazi kaunti ya Kwale sasa wanamtaka waziri mteule Salim Mvurya na mwenzake Ali Hassan Joho kueka kando tofauti zao za kisiasa na badala yake kushirikiana katika swala zima la kuhudumia taifa baada ya rais Wiliam Ruto kuwateuwa katika wizara ya biashara na uekezaji na ile ya madini na uchumi samawati mtawalia .
Kauli zao zinajiri baada ya rais Ruto kuvunja baraza la mawaziri siku chache zilizopita na kulifanyia mabadiliko ambapo Salim Mvurya ambae ameteuliwa kama waziri wa biashara na uekezaji aliishikilia wizara ya madini na uchumi samawati katika baraza lililopita.
Wakiongozwa na Hamisi Juma Shomali wameipongeza hatua ya rais Ruto kumrudisha katika wizara ,waziri Salim Mvurya ,wakiitaja hatua hio kuonyesha heshima kubwa kwa wakaazi wa Kwale na pwani nzima kwa ujumla .
“Wakati baraza la mawaziri lilipovunjwa sisi kama wa Kwale tulikuwa na wasiwasi sana kwa maana rais alipoteuwa upya mawaziri kwa awamu ya kwanza hakukuwa na mwakilishi kutoka eneo la pwani ,ila hadi sasa tunampongeza rais kwa kumteuwa waziri Mvurya na mwenzake Ali Hassan Joho hii ni heshima kubwa kwa wakaazi wa pwani ,” Asema bw Shomali .
Shomali aidha amemtaka waziri Mvurya na mwenzake Hassan Joho kuhakikisha wanaleta pamoja wakaazi wa eneo la pwani ,kwani muda wa siasa umepitwa na wakati .
“ Hatuwezi kueka taifa katika joto la kisiasa kila wakati ,tunataka mawaziri wetu mueke kando tofauti zenu za kisiasa na muhudumie wakenya kuambatana na kanuni za katiba ya nchi ,waziri Mvurya ujue sisi tunajivunia kama wa Kwale na tunataka wakati mnaposherehekea baada ya kuapishwa sherehe hio muifanye kwa pamoja hapa Kwale ili wapwani na Kenya kwa ujumla wathibitishe umoja wenu ,” Adokeza bw Shomali .
Kadhalka bw .Shomali amemsihi rais Ruto kuhakikisha aliyekuwa waziri wa jinsia Aisha Jumwa pia anapata nafasi kwa mara nyengine katika serikali ya Kenya Kwanza .
“ Ikiwa nafasi itapatikana rais umkumbuke dada yetu Aisha Jumwa na pia unyoshe Zaidi mkono wako hadi kaunti ya Lamu na uteuwe kiongozi ,naamini bado kuna nafasi katika serikali yako ,” Asema bw Shomali .
Mkaazi na mfanyibiashara aliyepia mkereketwa wa kisiasa Richard onsongo amemtaja waziri Mvurya kama kiongozi shupavu na mweledi wakutekeleza majukumu yake kwa wananchi.
“Uteuzi wa waziri Mvurya ni haki yake mana hii serikali ya Kenya Kwanza aliipigania ,kwa hio kuteuliwa kwake ni kwa halali na haki na ninashukru rais kwa kumteuwa ,waziri Mvurya aliwafanyia kazi wakaazi wa Kwale kwa kipindi cha miaka kumi akiwa gavana ,hivyo nina Imani kuwa wizara hii ya biashara na uekezaji pia ataiendesha kwa haki na uwazi kama alivyofanya alipokuwa katika wizara ya madini na uchumi samawati ,”Asema bw Onsongo .
Aidha amemtaka waziri Mvurya kueka mwafaka wakuleta waekezaji Zaidi nchini kama njiamojawapo ya kufungua nafasi za ajira kwa vijana hususan kaunti ya Kwale .
“ Hatuna waekezaji wakutosha na zaidi ni katika kaunti ya Kwale na hatua hio imewapelekea vijana kukosa ajira kote nchini ,tukipata waekezaji wakutosha vijana wetu watapata ajira ili wajiendeleze kimaisha na kuepuka vishawishi potofu ,” Aeleza bw. Onsongo .
Wakati uohuo amemtaka waziri wa madini na uchumi samawati Ali Hassan Joho kuiga nyayo za waziri Mvurya katika uendeshaji wa wizara hio ya madini .
“ Waziri Joho tunamuomba sana ushauriane na magavana ambao kaunti zao zina madini ili upate mwongozo wa jinsi shughuli za uchimbaji na sheria zinatekelezwa , hapa Kwale tuko na madini katika mlima wa Mrima huko Lungalunga kwa hio usikimbilie kuleta waekezaji na kuikandamiza jamii inayoishi pembezoni mwa mlima huo ,ninataka uje ushauriane na gavana Fatuma Achani kabla ya shughuli zozote za uchimbaji kutekelezwa ,”Asema bw Onsongo .
Pauline Wanja Kamau amempongeza rais Ruto kwa kumteuwa waziri Mvurya kwa mara ya pili japo kumtaka waziri Mvurya kuhakikisha anaboresha shughuli za kibiashara kaunti ya Kwale na taifa zima kwa ujumla .
“ Kusema ukweli sikuwa napata usingizi baada ya baraza la mawaziri kuvunjwa kwani nilimjua waziri Mvurya kama kiongozi mchapa kazi ,rais Ruto ameonyesha heshima kubwa kwa wakaazi wa Kwale kwa kumrudisha uongozi ,nina Imani atatuangalia sisi wamama mana tunapenda biashara sana ,tunataka hio pesa ya biashara na uekezaji itufaidi kikamilifu ,”Asema bi .Kamau.
Hata hivyo Mwasifa Omar Juma amewataka mawaziri wateule kufanya kazi kwa uadilifu badala ya kuingiza siasa za vyama .
“ Mawaziri walioingia kwa serikali wamheshimu rais Ruto wasije wakaharibu serikali kwani wakenya wanahitaji huduma bora sio chama bora ,tumeona mara nyingi aliyekuwa waziri mkuu Raila Odinga akipewa nafasi huvuruga serikali nakupelekea wakenya kukosa utulivu ,nina Imani wakati huu akipewa nafasi atadumisha nidhamu na kutoa nafasi kwa serikali kuwahudumia wakenya ,”Asema bw Mwasifa .
Kadhalka amemtaka rais Ruto kushirikiana na waziri mteule wa madini na uchumi samawati Ali Hassan Joho na yule wa biashara na uekezaji Salim Mvurya kutatua changamoto ya unyakuzi wa ardhi zilizoko pembezoni mwa fuo ya bahari eneo la pwani .
“Mambo ya ardhi zilizoko katika sehemu za bahari waziangalie zisinyakuliwe na mabwebwe na kuwafanya waekezaji kukosa sehemu za kufanikisha shughuli zao , waziri hataweza kufanyakazi wakati ardhi zimenyakuliwa na fuo za bahari kuchafuliwa ,” Asema bw. Mwasifa .
Kwa kauli moja wakaazi hao wameelezea matumaini yao kuwa hakuna waziri aliyeteuliwa atakayetupwa nje baada ya kupigwa msasa na bunge la kitaifa .





Comments
Post a Comment