ARDHI ILIYOCHIMBWA MADINI NA KAMPUNI YA BASETITANIUM KUTUMIKA KWA MIRADI YA MAENDELEO.
Taarifa yake : Caroline Katana
Wizara ya madini nchini inasema kwamba ardhi iliyochimbwa madini na kampuni ya Basetitanium haitarejeshwa kwa wenyeji.
Waziri wa madini Ali Hassan Joho ameshikilia kuwa ardhi hio itasalia katika himaya ya serikali kuu na kutumika katika maswala ya maendeleo ili kutoa nafasi za ajira kwa zaidi ya wafanyika elfu moja ambao watakosa ajira wakati kampuni hio itakapofungasha virago vyake mwisho mwa mwaka huu.
“Ardhi hii inaposalia katika usimamizi wa serikali ni sharti tuanze kufikiria maswala mseto ya utumizi wa ardhi hii kama vile uhifadhi msitu ,uzalishaji wa chakula cha mifugo ,kilimo cha ufunyuziaji na ufugaji samaki katika mabwawa yaliyopo ,” Asema waziri Joho.
Waziri Joho aliyekuwa akizungumza katika ziara yake ya kutathmini jinis zoezi la urekebishaji wa sehemu zilizochimbwa madini unavyotekelezwa ,asema kuwa ni sharti wenyeji wakomeshe tabia za kung’ang’ania kupimiwa ardhi hio kwa manufaa binafsi.
“ Ni lazima wakaazi waachane na fikira za kupata kipande cha ardhi cha 50 kwa 100 wakati kunapotokea nafasi ya ardhi ,shamba hili ni rasilimali ni wakati wa kufikiria maswala ya kimaendeleo ili kuhakikisha wenyeji wanajikuza kiuchumi ,watu wanaotoka katika kampuni hii ni wengi na kuna haja ya mipango thabiti kuafikiwa ili kutoa ajira ,” Asema waziri Joho.
Wakati uo huo ameonya dhidi ya uchochezi wa kisiasa katika swala la uteuzi wa kamati ya Post Mining Land Use kuwa hatua hio huenda ikasambaratisha malengo ya serikali ya kuikuza ardhi hio.
“ Sitovumilia uchochezi wa kisiasa wa aina yeyote katika swala muhimu kama hili , sio kila mtu atateuliwa katika kamati hio japo kuna nafasi ya kila mkaazi kutoa maoni , zoezi hilo litafanyika kwa mjibu wa sheria ,” Ahoji waziri Joho.
Akigusia swala la utoaji ruzuku ,waziri huyo amesema kuna haja ya kuwepo na mageuzi katika sheria ya ugavi wa ruzuku hio kuanzia kwa waathiriwa wa madini ,serikali ya kaunti na ile ya kitaifa.
“ Wizara yangu itafanya kazi kwa ukaribu na bunge la kitaifa ili kuhakikisha asilimia 10 ya wakaazi ,aslimia 20 ya serikali ya kaunti na asilimia 70 ya serikali ya kitaifa ya ruzuku ya madini inatolewa kwa wakati ,haina haja ya kuzuia fedha za watu ,” Asema waziri Joho.
Waziri Joho akiapa kushirikiana na wizara ya ardhi ,tume ya kitaifa ya ardhi na serikali za kaunti pwani kuwakabili mabwenyenye walionyakua ardhi za umma.
“Jimbo hili la pwani watu kunyakua ardhi za umma ni kawaida lakini sisi tumewapangia shamba la umma litarudi tu ,ardhi ni rasilimali inayomjenga mwananchi kiuchumi lazima tuhakikishe yanarudi kwa wananchi ,” Asisitiza waziri Joho.
Kwa upande wake naibu gavana wa Kwale Josphat Chirema Kombo amesema kuwa malengo ya serikali ya kaunti ya Kwale ni kuhakikisha jamii inafaidika kikamilifu na miradi ya maendeleo hivyo kusisitiza umuhimu wa kutupilia mbali siasa zisizo na msingi .
“ Serikali ya Kwale iko imara na malengo ni kuhakikisha kuwa wanaelekeza fikira zao kwa wafanyikazi ambao watapoteza ajira , ardhi hii sio ya kabila moja ardhi hii sasa ni ya serikali ambayo kila faida ni lazima iwe faida ya wakaazi ,”Asema naibu Chirema.
Kiongozi huyo akihoji kuwa zoezi la umma la utoaji maoni kuhusiana na utumizi wa ardhi hio ni kwa manufaa ya wakaazi.
“ Kuhusishwa kwa wananchi katika zoezi hili ni muhimu sana ,katika mradi huu watu wanaelewa kuwa tumekuwa watu wakuzungumza na wakaazi ,kila hatua tunayochukua kama serikali ni kwa manufaa ya wakaazi kwa hio hatutarusu siasa ya aina yeyote ,”Asema naibu Chirema.
Aidha ameelezea kuridhishwa kwake na jinsi usimamizi wa kampuni ya Basetitanium unavyopiga jeki Agenda ya rais William Ruto ya kupanda miti katika ardhi hio.
Hata hivyo naibu Chirema ameitaka wizara ya madini kushirikiana kwa ukaribu na serikali ya kaunti katika swala la utoaji mwongozo wa utumizi wa ardhi hio.
“ Kama ni siasa tafuteni Agenda nyengine ,mambo ya Basetitanium na hii ardhi tuachie wizara itupange ,”Asema naibu Chirema.
,Mbunge wa Msambweni Feisal Bader amemtaka waziri Joho kuhakikisha kamati teule ya kusikiza maoni ya wakaazi kuanza kazi mara moja kwani muda wao unakaribia kutamatika ,kulingana na mkataba wa hapo awali uliokwa na aliyekuwa waziri wa madini Salim Mvurya unakamilika mwezi Desemba mwaka huu.
Nae mbunge wa Matuga Kassim Tandaza ameutaka usimamizi wa kampuni ya Basetitanium kuhakikisha wanafuata sheria zilizopo hadi watakapokamilisha muda wao .
Kwa upande wake mbunge wa Lungalunga Mangale Munga Chiforomodo ametoa changamoto kwa serikali kupitia wizara ya madini kujenga chuo cha mafunzo ya shughuli za uchimbaji madini na taasisi ya utafiti katika ardhi hio.
Spika wa bunge la Kwale Seth Mwatela Kamanza akisema kwamba bunge la Kwale litahakikisha sheria hitajika za kusaidia katika zoezi zima la utumizi wa ardhi hio zinaangaziwa kikamilifu.
.jpg)
.jpg)
Comments
Post a Comment