DINI NI AMANI SIO MISIMAMO MIKALI.
Leo hii dunia imekuwa ni uwanja wa fujo ,vurugu na ghasia ,watu wanateseka kutokana na misimamo mikali ya kidini na kiimani .
Matamanio ya wengi ni kiu ya amani ,matumaini ,kwa kusimama kidete ,kulinda utu wa binadamu ,kutafuta na kudumisha ustawi ,maendeleo na mafao ya wengi kwa kuoneshana huruma na upendo pamoja na utunzaji bora wa mazingira nyumbani.
Uhuru wa kidini unafumbatwa katika mambo makuu matatu kama vile umuhimu wa kujenga na kudumisha umoja na mshikamano miongoni mwa waamini wa dini mbali mbali ,kulinda na kudumisha amani na utulivu kama chachu muhimu ya ustawi ,majadiliano ya kidini katika ukweli na uwazi ni mbinu mkakati unaoweza kuleta suluhu ya migogoro mingi.
Uhuru wa kidini unapaswa kuzingatiwa na kuendelezwa kisheria kwa maana ni haki msingi za binadamu zinazopaswa kulindwa na kuendelezwa kwa kuheshimu na kutthamini dhamiri ya mtu binafsi na jamii katika ujumla wake.
Katika juhudi hizo shirika la kijamii la Kenya Community Support Centre KECOSCE limejizatiti katika kasi za kuleta uiano na utangamano miongoni mwa viongozi wa kidini kaunti ya Kwale na maeneo mengine ya nchi kupitia mradi wa Joint Initiative for Strategic Religious Action JISRA.
Mradi huo wa JISRA wa miaka mitano ukitekelezwa katika mataifa saba ,Kenya Ethiopia ,Indonesia ,Iraq, Mali ,Nigeria na Uganda.
JISRA huchochea nguvu chanya ndani na kati ya jumuiya za kidini kwa jamii zenye amani na umoja Zaidi.
JISRA inaboresha jukumu la kuwajenga watendaji wa kidini ,mpango huu unashughulikia kanuni na masimulizi yenye madhara ndani ya jumuiya za kidini, huchochea ushirikiano kati ya dini na kuonyesha kwamba mila mbali mbali za kidini zinaweza kukusanyika pamoja katika maono ya pamoja kwa ajili ya jamii bora na ya haki.
JISRA inatoa kipaumbele maalum katika kuongeza nafasi ya wanawake na vijana katika kuweka dira na ufumbuzi wa kuendeleza na kukuza ushiriki wa vijana na wanawake katika vikao vya maamuzi.
Kwa kuzingatia kifungu cha 18 cha tamko la kimataifa la haki za kibinadamu kuhusu uhuru wa dini na Imani ,JISRA inachangia lengo la 16 la maendeleo endelevu, (kukuza jamii zenye haki ,amani na shirikishi) na lengo la 5 la maendeleo endelevu (kufikia usawa wa kijinsia wa kuwawezesha wanawake na wasichana wote).
Afisa wa nyanjani wa mradi wa JISRA katika shirika la kijamii la Kenya Community Support Centre KECOSCE Mwalimu Rama aliyekuwa akizungumza alipokutana na baadhi ya makundi ya kijamii yaliyofaidika na mradi wa Participatory Grant Making kupitia mradi wa JISRA kaunti ya Kwale, ametoa changamoto kwa viongozi wa kidini na makundi yaliyofaidika kuhakikisha uendelevu wa mradi huo ili jamii ziweze kuishi kwa amani.
“Tunaona elimu ya JISRA imewafikia wanajamii na tunaomba hii elimu iendelezwe ili kuleta uiano na kukabiliana na mihemko ya maswala ya itikadi kali inayovuruga amani ,kwa hio natoa wito kwa wale waliofikiwa na mradi huu kuwa mabalozi na kusambaza elimu hii kwa wote ambao hawakufikiwa ,”Asema bw. Rama.
Bw.Rama aidha amewataka viongozi wakidini na asasi za usalama kutekeleza majukumu yao kikamilifu badala ya kufumbia macho changamoto zinazoisibu jamii.
“Tunataka kuona wachungaji wakitoka makanisani ,masheik watoke misikitini na maafisa wa usalama watoke afisini waje nyanjani kuizungumzia jamii umuhimu wa kudumisha amani na kuishi na uiano na utangamano , tunaona kuwa mfumo huu utawawezesha vijana kubadilisha mienendo yao ya uovu na kuwazalendo na kuhakikisha amani endelevu ,”Asema bw. Rama.
Wakati huo uo amewataka vijana kujitenga na vishawishi potofu kutoka kwa viongozi wa kisiasa.
“Vijana wakipewa pesa na mwanasiasa kwa lengo la kuzua vurugu , wachukue pesa hizo na wazitumie kwa njia ya kujiendeleza badala ya kuwasikiza wanasiasa na kuzuia ghasia ,tuna Imani hatua hii itawafanya wanasiasa wabadilishe tabia zao za kuwatumia vijana kwa misingi potofu ,”Asema bw. Rama.
Kadhalka bw. Rama ameelezea matumaini yake ya mradi huo kuendelezwa kwa jamii hata baada ya kukamilisha muda wake wa miaka mitano mwaka ujao.
Mwanahamisi Athman anayeshughulikia maswala ya akinamama wachanga eneo la Waa ameafiki akinamama hao wachanga kupitia changamoto msingi katika jamii.
“Msichana akijifungua mapema jamii humshusha hadhi badala ya kumjenga kimaisha ,nafasi ya kuongea katika jamii huwa finyu mno hatua ambayo inatunyima nafasi ya kutetea haki zetu katika jamii ,”Asema bi. Athman.
Bi. Athman akitoa changamoto kwa mashirika mbali mbali ya kijamii kuwahusisha kikamilifu katika vikao vya kuwajenga uwezo na utetezi ili waweze kujiimarisha kimaisha ,akihoji kuwa sasa jamii imeanza kuchukua mtazamo tofauti dhidi yao tangu aanzishe mradi wa kuihamasisha umuhimu wa kulinda haki za watoto wakike.
Hata hivyo bi. Athman amewataka watoto wakike kujiepushe na ngono za mapema ili kuepuka mimba na ndoa za utotoni zinazozima ndoto zao za ufanisi katika maisha ya usoni.
Mwalimu wa madrassa ya Munawar Tiwi Chai ,ustadha Mariam Said Mohamed amesisitiza umuhimu wa wazazi kuwakuza waoto wao katika misingi ya kidini ili kuhakikisha wanakua na maadili mema.
“Mtoto akikuzwa kwa misingi ya dini anaepuka vishawishi vingi vya kidunia ,mana dini inakataza uovu ,”Asema bi.Mohamed.
Hata hivyo mwalimu huyo ameafiki kukumbana na changamoto nyingi zinazowakabili watoto ambazo zinaonekana kutelekezwa na wazazi.
Mashirika ya kijamii yaliyofaidika na mradi wa JISRA kupitia Participatory Grant Making PGM kaunti ya Kwale ni pamoja na lile la Green minds ,Ched, smart move, 2ko na hope na Kwale women desk.
Comments
Post a Comment