MAONO YA MSICHANA KWA SIKU ZIJAZO
Taarifa yake : Caroline Katana
Maono ya msichana kwa siku zijazo ndio kauli mbiu ya siku ya maadhimisho ya siku ya msichana duniani ,ambayo kaunti ya Kwale imesherekewa katika kijiji cha Bwiti ,eneo bunge la Lungalunga ,Jamii ikitakiwa kutia kasi Zaidi katika swala zima la kuripoti visa vya dhulma za kijinsia dhidi ya mtoto wakike ili waathiriwa wapate haki kwa wakati ufaao.
Mkurugenzi wa shirika la kijamii la Tuwajali Wajane Kwale a mbae pia ni mtetezi wa haki za akinamama wajane ,watoto na wasichana Mwanasha Gaserego amesema kuwa ni sharti jamii iwe na mfumo thabiti wa kufichua kesi hizo ili washukiwa wakabiliwe kisheria.
Bi .Gaserego aliyekuwa mgeni mashuhuri katika sherehe hio amehoji kuwa lazima maono ya mtoto wakike yaafikiwe kikamilifu katika jamii .
“Siku hii ina umuhimu mkubwa sana katika jamii kwa sababu bila maono haina haja ya kuishi katika hii dunia , nina imani hii hamasa ya siku ya leo kutakuwa na mabadiliko katika jamii dhidi ya kuripoti hizi kesi za dhulma za watoto hususan msimu huu wa likizo ndefu ,”Asema bi .Gaserego.
Bi. Gaserego akizitaja kesi za ngono jamii kujitokeza katika dawati la kijinsia la kituo cha polisi cha Msambweni.
“ Akinamama wanaosafiri Ughaibuni kutafuta ajira huacha nyuma watoto wao na wanajamii ambao badae huwageuka na kuwafanyia vitendo vya ukatili ,kesi hizi zinaripotiwa sana kufuatia hamasa inayotolewa mashinani kuhusiana na athari za dhulma za kingono kwa watoto ,” Asema bi. Gaserego.
Bi . Gaserego aidha ametoa wito kwa mashirika mbalimbali ya kijamii na serikali kufanya kazi kwa pamoja ili kufanikisha maono ya mtoto wakikeKadhalka kiongozi huyo ametoa changamoto kwa serikali ya kaunti ya Kwale kutafuta mwafaka wakifedha ili kuhakikisha sheria ya kijinsia ya mwaka 2023 inatekelezwa baada ya kukosa kutengewa bajeti katika mwaka huu wakifedha.
“ Kuna haja ya serikali ya kaunti kutafuta fedha kupitia ushuru wa ndani kama vile sekta ya utalii , kilimo na ufadhili wa mashirika ya kimataifa ili kuitekeleza sheria hio badala ya kutegemea fedha kutoka kwa serikali ya kitaifa ,” Asema bi. Gaserego.
Hata hivyo ameelezea hali ya msichana kaunti ya Kwale kuzidi kuimarika kinyume na ilivyokuwa hapo awali kufuatia fursa zilizopo kama ufadhili wa masomo kutoka serikalini na mashirika yasiyokuwa yakiserikali kama ufadhili wa Wings to Fly kutoka kwa benki ya Equity.
Afisa wa watoto eneo bunge la Lungalunga Elizabeth Kariuki ameafiki visa vya dhulma kwa watoto kuripotiwa kwa wingi katika afisi yake baada ya jamii kuhamasishwa kuhusiana na haki za watoto.
Mimba za utotoni , unajisi ,ajira za utotoni na watoto kukosa haki msingi ya elimu akizitaja kama changamoto zilizokithiri katika eneo bunge hilo la Lungalunga.
Bi.Kariuki akisema kuwa utekelezaji wa sheria ya kijinsia 2023 utasaidia pakubwa kukabiliana na dhulma za kijinsia kaunti ya Kwale.
Kivuli Johnstone afisa wa watoto eneo bunge la Msambweni ametaja swala la wazazi kuwaachilia watoto wao kuwa changamoto sugu.
“Sheria ya watoto 2022 inatambua uwachiliaji wa watoto ,ikipita muda Fulani bila ya mtoto kuwa na wazazi wake ,kulingana na sheria mzazi amewaachilia watoto wake ,tunaona ya kwamba watoto wengi ambao wazazi wamesafiri nchi za nje wameachiliwa ndio maana wengi wao wanadhulumiwa kingono na watu wao wakaribu ,”Asema bw.Kivuli.
Afisa huyo wa watoto sasa anawataka wazazi wanaotafuta ajira Ughaibuni kuhakikisha wanaacha watoto wao katika mikono salama badala ya kuwaachilia kuwa hatua hio ina kiuka haki za watoto.
Mwenyekiti wa kikundi cha Girls Acts Program Muema Joan ameelezea furaha yake ya kutambulika kwa mtoto msichana akisema kuwa wanaendeleza mpango wa kuwahamasisha wasichana kutoka jamii zisizojiweza umuhimu wa kusoma na kukamilisha masomo yao jinsi ya kujiepusha na mimba za utotoni pamoja na kuwasaidia na kuwajenga uwezo wasichana waliopata maambukizi ya virusi vya ukimwi .
Bi .Muema akiitaka jamii kutambua haki za mtoto wakike badala ya kuwatelekeza kuwa hatua hio imepitwa na wakati .
“ Mtoto wakike akielimika jamii nzima ime elimika ,wazazi waachane na tamaduni potofu dhidi ya mtoto wakike ,ni sharti haki msingi za watoto zipewe kipao mbele katika jamii ili kuhakikisha wanakua katika mazingira salama ,” Asema bi .Muema .
Shirika lisilokuwa la kiserikali la Aids Healthcare Foundation Kenya lilianza kufanya kazi mwaka 2007 na kusajiliwa rasmi kama NGO ya kitaifa inayofanya kazi nchini kenya mnamo Juni 2008 .
Mipango ya AHF Kenya inaendeshwa kwa ushirikiano na washirika ,wizara ya afya na serikali za kaunti ,lengo kuu ni kuwa na huduma bora kwa wakenya bila gharama yoyote .
AHF Kenya inaunga mkono mpango wa kuzuia magonjwa mbalimbali unaojumuisha ufikiaji wa kila mwezi wa upimaji wa HIV bila malipo na ushauri nasaha katika jamii nyingi ambayo inaruhusu maafisa kutambua watu wanaoishi na HIV ambao wako nje ya huduma kwa kuwaunganisha na huduma.
Muuguzi katika shirika hilo la AHF anayetekeleza programu ya Girls Acts Lucy Mugambi amesema kuwa programu hio inahusika na maswala ya msichana wa kati ya umri wa miaka 10 hadi 24.
“Tunafanya mambo matatu ,kuangazia elimu ya mtoto wakike hadi akamilishe masomo ,kuzuia mimba za utotoni na kuhakikisha mtoto wakike hapati maambuzi mapya ya virusi vya ukimwi ,” Asema bi.Mugambi.
Aidha amedokeza kuwa kulingana na takwimu watoto wakike wa kati ya umri wa miaka 10 hadi 24 wako katika hatari ya kupata maabukizi ya virusi vya ukimwi kufuatia na visa vya dhulma za kingono wanavyokumbana navyo katika jamii.
“ Tumeweza kuelimisha watoto wetu ili waweze kuzuia mimba za mapema ,wasome wakamilishe masomo yao ,tunawapatia ufadhili wa masomo na sodo ili kuwaepusha na vishawishi vinavyowaponza katika maisha yao ,” Asema bi.Mugambi.
Comments
Post a Comment