KITUO SALAMA CHA WATOTO KURIPOTI KESI ZA DHULMA CHA ZINDULIWA MSAMBWENI ,KWALE .
Taarifa yake : Caroline Katana
Katika juhudi za kuhakikisha mazingira salama ya kutoa taarifa za kesi za dhulma za kijinsia , shirika la kimataifa la kukomesha dhulma dhidi ya wanawake na watoto International Justice Mission, Kenya kwa ushirikiano na asasi za usalama kaunti ya Kwale ,wamefungua rasmi kituo salama cha watoto ( child protection unit ) katika kituo cha polisi cha Msambweni kaunti ya kwale.
Hii ni baada ya kesi za dhulma dhidi ya watoto kuzidi kuripotiwa kila mwaka katika kaunti hio , eneo hilo la Msambweni likinakili visa vingi Zaidi vya unajisi wa watoto kati ya visa vilivyoripotiwa kaunti ya Kwale mwaka huu.
Kulingana na takwimu zilizotolewa na kamanda wa polisi kaunti ya kwale Ali Nuno mwaka 2022 hadi 2024 jumla ya kesi 381 za unajisi wa watoto zilinakiliwa.
“Mwaka 2022 tulirekodi jumla ya kesi 111 , 2023 kesi 147 zilirekodiwa na 2024 kesi 123 zimerekodiwa ,kesi zote zikiwa za unajisi na eneo bunge la Msambweni likiongoza kwa visa 60 kati ya visa vyote vilivyoripotiwa mwaka huu ,hivyo naeza sema kulingana na takwimu hizi ,Msambweni ni eneo ambalo ni hatari kwa usalama wa watoto ,”Asema bw.Nuno.
Nuno aliyekuwa akizungumza wakati wa uzinduzi wa kituo hicho ametaja ndoa na mimba za mapema , utalii wa ngono kwa watoto ,unyanyasaji wa watoto ,ukeketaji na vitisho vya ngono kwa watoto hususan katika eneo la Diani kuwa changamoto sugu .
“Ni lazima tuwe macho Zaidi katika swala la kuwalinda watoto wetu , mazingira tunayofanyia kazi yanaeza kuwa sio salama kwa watoto hivyo ni sharti tutie juhudi Zaidi za ulinzi wa watoto ,” Asema bw.Nuno .
Aidha afisa huyo wa usalama amehoji kuwa kituo hicho kitakuwa na mchango mkubwa wa kukabiliana na changamoto msingi zinazokiuka haki za watoto .
“Kituo hiki kitatoa mazingira salama kwa waathiriwa kutokana na kuripoti kesi za dhulma bila uoga na kwa siri ,ili kuhakikisha haki na ulinzi wa watoto waliodhulumiwa.
Wakati huohuo amewataka watetezi wa haki za watoto kuondoa hofu na uoga katika utendakazi wao ,akitoa hakikisho la kuwalinda watetezi wa haki ili kufanikisha shughuli zao za kuwafichua washukiwa .
“ Msiogope vitisho ,tutahakikisha mko na usalama wa kutosha ,kwa hio nawasihi muendeleze juhudi hizi za kulinda na kutetea haki za watoto kikamifu ,” Asema bw. Nuno.
Hata hivyo amewataka wazazi kusitisha tabia za kusuluhisha kesi za dhulma za watoto kinyumbani na badala yake kushirikiana kwa ukaribu na asasi za usalama ili kukomesha visa hivyo .
Hakimu wa mahakama ya Msambweni Leah Kabaria amesema kuwa kuna haja ya umma kufahamu sheria na haki za watoto.
“ Hukumu ya kesi za dhulma za kingono kwa watoto ziko juu sana ,lakini ukiona kwamba hukumu iko juu na bado watu wanashtakiwa kwa kosa hilo ,ina maana kuna kitu hatujafanya ,la kwanza ikiwa ni kufahamisha umma kuhusu haki za watoto ,” Asema hakimu Kabaria .
Bi. Kabaria amesema kuwa bado kuna ugumu wa kuripoti kesi za dhulma za kingono kwa watoto hususan zile za ngono jamii .
“Kama mtoto amenajisiwa na baba yake mara nyingi haziripotiwi mana zinatajwa kuwa ni kesi za aibu ,ni sharti tulete mwangaza kwa kesi hizi na tuondoe aibu ,mmefunguliwa kituo hiki leo ,waathiriwa watakuwa na mahali salama kwa kuripoti kwa hio tusinyamazie uovu wa aina yeyote ,tusiwe na vikao pale nyumbani vya kusuluhisha kesi hizi ,tuziripoti ili haki kwa waathiriwa ipatikane ,” Asema bi .Kabaria
Hakimu Kabaria amewataka wadau mbali mbali kushirikiana katika juhudi za kukomesha dhulma za kijinsia.
Afisa wa shirika hilo la IJM Kalisto Badia amesema kuwa kituo hicho chenye vyumba vine kitatoa huduma ya ushauri , mahojiano , dawati la maswala ya kijinsia na sehemu ya familia za waathiri kusubiri watoto wao kuandikisha taarifa.
Wakati uo huo afisa wa IJM Naomi Maina ametaja umuhimu wa jamii kurudi katika misingi ya malezi ya watoto.
“ Mtoto akilelewa vizuri , wakati akikomaa hatakuwa na mawazo ya kutenda uovu ,ili kukomesha visa vya dhulma za kijinsia kama jamii ya hapa Msambweni na Kwale nzima kwa ujumla ni kutafuta mwafaka wa jinsi ya kujirudi na kuboresha mifumo ya kijamii ya malezi ,”Asema bi .Maina
Bi .Maina amesisitiza umuhumu wa wadau kushirikiana na kuripoti kesi hizo pamoja na kuendeza mijadala ya vipi wataweza kuwakinga watoto dhidi ya visa hizo .
Kadhalka ameeleza kuwa IJM inaendelezea kuboresha mfumo wa haki za jinai katika kukabiliana na kuzuia unyanyasaji wa wanawake na watoto nchini kenya .
Comments
Post a Comment