SERIKALI NI SEHEMU YA MIZOZO YA ARDHI NCHINI INA UUZA NA KUPORA ARDHI ZA UMMA.
Taarifa yake : Caroline Katana
Changamoto ya migogoro ya ardhi nchini zinazidi kuwa kubwa kila uchao ,ipo mizozo kati ya wafugaji na wakulima ,wananchi dhidi ya serikali ,wananchi dhidi ya wawekezaji kwa nyakati zote waathirika ni wananchi ambao ndio wanaopoteza haki zao za kutumia ardhi.
Mara nyingi tumeshuhudia mauwaji ,mapigano ,kufukuzwa na kuondolewa kwa wananchi kwenye ardhi zao.
Pamoja na migogoro kuwa mingi nchini ,kasi ya utatuzi ni ndogo sana na kwa maeneo mengine njia za utatuzi hazifanyi kazi kwa ufanisi .
Serikali ni sharti iache udalali wa kupora na kuuza ardhi za wananchi kwa kisingizio cha kuzikodi kwa wawekezaji.
Wakaazi wa Kanana , Nguzo ,Pongwe, Kidimu na Nikaphu wako katika njia panda baada ya serikali kukodi ardhi ya jamii kwa kiwanda cha uzalishaji sukari cha KISCOL huku ahadi ya kuwaondoa wenyeji hadi katika ardhi mbadala ikisalia kuwa hewa.
Wakati serikali ikikodi ardhi hio tayari wakaazi hao walikuwa wanaishi kwenye sehemu hio yenye hekari 800 na kuitumia kwa ajili ya shughuli za kilimo.
Kuanzia hapo mwekezaji huyo alianza shughuli zake za upanzi wa miwa ili kutimiza azma yake ya kufanikisha biashara ya uuzaji sukari.
Mwaka 2018 wakaazi hao na mashirika ya kutetea haki za kibinadamu walitafuta haki mahakamani na hukumu kutolewa mwaka 2023 ambapo serikali iliagizwa kuwaondoa wakaazi hao hadi katika ardhi mbadala pamoja na kuwafidia hasara ya mimea yao.
Salim Kassim Shee mkaazi wa kijiji cha Nikaphu anasema kuwa serikali inakuika haki zao.
“Wakati mahakama ilitoa maamuzi yake ,serikali ilipewa muda wa mwaka mmoja kutuondoa na kutulipa ridhaa zetu lakini hadi sasa ni mwaka wa pili na hakuna hatua yeyote inayochukuliwa , serikali ilichukua ardhi yetu ikapeana kwa mwekezaji wakati sisi ndio wamiliki halali na hadi sasa inatuchezea mchezo wa danganya toto ,”Asema bw.Shee.
Hatua ya mwekezaji huyo kupanda miwa hadi katika makaazi yao wakiitaja kuhatarisha maisha yao baada ya nyoka wenye sumu kali kupata makao katika bustani hio ya miwa.
Bw. Shee akiafiki watu watatu kufariki kufuatia mashambulizi ya nyoka ,kisha cha hivi majuzi kikiwa cha mtoto mwenye umri wa miaka 13 ,mwanafunzi wa gradi ya 5 katika shule ya msingi ya Genesis Kanana kufariki siku ya Jumamosi kufuatia shambulizi la nyoka.
“ Tunasikitika kuona sisi waathirika wanafariki kufuatia mashambulizi ya nyoka ,huyu mtoto sio wa kwanza ,sasa tunaishi kwa kuhofia usalama wetu ,hii shida ilianza mwaka wa 2018 walati wa serikali ya Uhuru –Ruto ,rais William Ruto alipoingia mamlakani akaahidi kutatua mizozo ya ardhi ila hadi sasa shida zinaongezeka kila uchao ,”Asema bw.Shee
Ardhi hio ya jamii ilipeanwa kwa mwekezaji huyo wa sukari kupanua shughuli zake ili jamii iweze kufaidika na ajira ili kujiinua kiuchumi jambo ambalo halijafanyika hadi sasa .
Bw. Shee akisema kuwa mahakama iliamuru serikali kuwafidia wakaazi hao ekari 5.5 pamoja na ridhaa ya mimea yao hatua ambayo imesalia kuwa stori za abunuasi .
Ginora Kinyasi akisema kuwa kuendelea kuishi katika eneo hilo kunazidi kuhatarisha maisha yao kutokana na ongekezo la nyoka hao ambao wamekuwa wakizurura katika makaazi kutafuta maji kutokana na makali ya kiangazi.
Kadhalka bi .Ginora amelitaka shirika la uhifadhi wa wanyamapori kubuni mbinu za kitenolojia za kuwanasa wanyama hao hatari ili kunusuru maisha yao wakati wanaposubiria kuondolewa katika eneo hilo.
“Tumechoka kulala na nyoka kwa majumba yetu ,wako na madhara makali na huku kwetu changamoto ya hospitali na barabara imekuwa kikwazo kikuu cha majeruhi wa nyoka kupata huduma za haraka ,tumeona katika eneo la Mwingi watu wanakatwa mikono na miguu kufuatia mashambulizi ya nyoka ,”Asema bi .Ginora .
Charity Halima lewa mama aliyempoteza mwanawe kufuatia shambulizi la nyoka anasema kuwa mwendazake Jacob Zuma Mwero alikumbana na mauti yake alipokuwa akijisaidia katika shamba hilo la miwa linalo milikiwa na KISCO.
Aidha ameitaka serikali kuhakikisha haki ya kila mkaazi inalindwa kwa mjibu wa katiba.
Familia hizo zisizopungua 600 kwa kauli moja zinamtaka rais William Ruto kutekeleza agizo la mahakama la kuwaondoa katika eneo hilo na kuwapeleka katika ardhi mbadala iliyo na usalama wakutosha ama asitishe kodi ya mwekezaji huyo na ardhi hio kwa mara nyingine iwafaidi wenyeji.
“Kama hakuna ardhi mbadala ambayo serikali inaweza kutupeleka ili tuishi kwa amani kama wakenya wengine basi watulipe ridhaa ya mimea yetu kisha watupimie hii ardhi yetu ,mana kufikia sasa tuko kwenye njia panda hatujui twende wapi tunaishi kwa ardhi hii na tumezungukwa na miwa kila upande hatuna hata mashamba ya kulima ,wakati wa kampeni alisema serikali yake ni kusema na kutenda ,sasa tunahitaji kuona vitendo sio kusema tu ,”
Haya yanajiri baada ya rais William Ruto katika hotuba yake wakati wa maadhimisho ya sherehe za mashujaa kusema kuwa tayari ametenga bajeti ya kushughulikia maskwata humu nchini.

Comments
Post a Comment