Makala ya soka ni amani, sio nguvu mtaani.
Taarifa yake: Caroline Katana
Mataifa mengi ya Afrika yamekuwa yakikabiliwa na changamoto za kiusalama ,makundi yenye silaha yakionekana kuongezeka licha ya juhudi za serikali za kikanda na ukanda kuimarisha usalama pamoja na kutuma vikosi vya polisi kuyakabili makundi yenye silaha.
Serikali barani afrika hutunga sheria ,kuweka kamera za siri ,kuongeza na kuimarisha vikosi vya mafisa wa usalama katika maeneo hatari ,hata hivyo ingawa mbinu hizo hufaulu kwa kiwango Fulani ,bado hazitatui chanzo hasa cha tatizo ,ukweli ni kwamba matendo ya watu hutegemea tamaa zao,mtazamo wao na mambo wanayoamini .
Tuliishi maisha ya kawaida mwanzoni ,hatukuwazia kuvamiwa na wezi wenye silaha lakini sasa hakuna usalama tena ,iwe mjini au kijijini ,kuporomoka kwa uchumi kumefunua kwamba watu ni wenye pupa na hawaheshimu uhai wala mali za wengine .
Taifa la Kenya ni miongoni mwa mataifa duniani yanayoendelea kushuhudia idadi kubwa ya vijana wanaojiunga na magenge ya uhalifu ,licha ya kueka mikakati ya kuimarisha usalama wa nchi pamoja na kujaribu kubuni mbinu za kuboresha maisha ya vijana ,kaunti ya Nairobi ikionekana kuongoza na magenge ya uhalifu .
Ukweli ni kwamba amani na usalama inaweza boreshwa kwa kutumia akili na ujuzi wala sio kutumia nguvu kupita kiasi .
Je unaamini kwamba binadamu wana uwezo wakutatua matatizo yanayofanya tukose amani na usalama na yanayohatarisha maisha yetu ya wakati ujao ? tunahitaji kushughulikia chanzo au mzizi wake na sio dalili .
Eneo la pwani mwa Kenya ni eneo lililo na historia ya mchipuko ya makundi kama vile Kaya bombo na vuguvugu la Mombasa Republican miongoni mwa mengine yaliyodai kuikomboa pwani dhidi ya dhulma za kihistoria , japo kusababisha umwagikaji wa damu na kuhujumu amani na usalama .
Kaunti ya Kwale ni miongoni mwa kaunti za pwani ambazo zingali kushuhudia magenge ya vijana wenye umri mdogo wanaojihusisha na uhalifu na kutatiza amani na usalama miongoni mwa wenyeji na wageni wanaozuru eneo hilo .
Utafiti uliofanywa na shirika la kijamii la Samba sports youth Agenda dhidi ya vijana wanaojiunga na magenge hayo ukionyesha kuwa ,ukosefu wa ajira ,elimu ,kuvunjika kwa familia ,utumizi wa dawa za kulevya ,kisasi ni kati ya sababu zinazowachochea vijana wenye umri mdogo kujiunga na magenge ya kihalifu .
Kutokana na ubobeaji wa kitaaluma katika Nyanja ya kujenga ya amani katika jamii ,shirika la Sambasports Youths Agenda lilibuni mikakati mbalimbali ikiwemo kutoa pembejeo za kibiashara kwa makundi mbali mbali ya vijana ,hamasa za amani na usalama katika maeneo ya maskani ya vijana na hatimaye kuanzisha dimba la soka ili kuwanasua vijana katika jinamizi la uhalifu na kujenga amani .
Kujenga amani ni kati ya nguzo tatu muhimu zinazolengwa katika tamasha la MR.and MRS Samba 2024 , vijana wenye umri wa miaka 18 hadi 25 watapata fursa ya kuonyesha vipaji na ujuzi mbalimbali kama njiamowapo ya kuuza vipaji vyao kwa wafadhili katika kilele cha tamasha hilo tarehe 21 mwezi huu .
Mkurugenzi mkuu wa shirika la sambasports youth agenda Mohamed mwachausa akisema kuwa vijana 400 kwale wanatarajiwa kujiunga katika tamasha hilo ili kuonyesha vipaji vyao vyenye maudhui mbalimbali kupitia ,tamaduni ,mashairi ,nyimbo na michezo ya kuigiza.
“ Kabla ya matasha la MR.and MRS Samba kutakuwa na mafunzo ya kujenga amani peace , haki ya mazingira na afya ya uzazi na haki na afya ya akili ,mafunzo hayo ni kama kuwajenga hifadhi kwenye vifua vya hawa vijana ,ambao badae watatengeza miradi yao ambayo katika tamasha la Mr and Mrs Samba wataionyesha kwa wafadhili mbalimbali kama njiamoja wapo ya kuwafungulia njia ya kupata pembejeo ya kutekeleza miradi yao katika jamii ,”Asema bw. Mwachausa .
Akigusia swala la mabadiliko ya tabia nchi ,mwachausa amesema licha ya fuo ya bahari ya Diani kupata umaarufu kwa miaka minane mfululizo kuna haja kubwa ya kuilinda dhidi ya uchafuzi ili kuwavutia watalii Zaidi .
Hata hivyo amehoji kuwa kilele cha tamasha hilo ni kupata wafadhili watakaowezesha washindi wa miradi mbalimbali kuitekeleza katika jamii ili kuhakikisha jamii salama .
Kutoa hamasa ya kujenga amani kupitia soka kukiwaleta pamoja vijana kutoka vijiji 21 Matuga na Msambweni ambao awali walikuwa na historia zisizoridhisha .
Bw.Mwachausa akisema kuwa soka hio imekuwa ikichezwa kwa mtindo wa kipekee, kila baada ya dakika 40 vijana hukaa kwenye mahema na kuzungumziwa kuhusu umuhimu wa kujenga amani na kuishi kwa uiyano kama jamii moja.
“ Tukiangalia maeneo kama Kiteje ,Ng’ombeni ,Denyenye, Waa, Tiwi ,Bongwe- gombato ,Mulungu nipa na Kinondo kumekuwa na dosari ya vijana kujiingiza katika magenge ya kihalifu ,utumizi wa mihadarati na kufanya vitendo vya kuhujumu usalama na soka hii ya kujenga amani inalenga haswa vijana wa maeneo hayo ,”Asema bw. Mwachausa .
Mkurugenzi huyo akihoji kuwa soka ya kujenga amani imeleta uhusiano mwema kati ya vijana na jamii kwa ujumla kinyume na ilivyokuwa hapo awali ambapo haikua rahisi kwa vijana hao kuwa pamoja pasi na uwepo wa maafisa wa polisi .
“ Eneo kama la Ng’ombeni haikuwa rahisi kufanya michezo kufuatia historia ya vita ,ghasia , ilikuwa ni lazima watu waandamane na maafisa wa usalama ili kufanikisha shughuli zao ,lakini tangu tuanze mpango huu wa kujenga amani kupitia soka na midahalo ,vijana wamebadilika na tamasha zetu za michezo zinafanyika bila hata kusimamiwa na maaskari gongo na hii ni hatua kubwa sana ya ufanisi kwa jamii ya eneo la Ng’ombeni ,”Asema bw.Mwachausa
Mchezaji wa Kalamu FC Suleiman Abdallah kutoka kijiji cha Mwamanga eneo bunge la Msambweni ni kati ya mamia ya vijana waliofaidika na mradi wa kujenga amani unaotekelezwa na shirika la samba sports youth agenda ,ambaye hadi kufikia sasa amekuwa balozi wa amani.
Abdallah ambaye alianza kucheza soka na timu ya Ukunda Sport Academy akiwa na umri wa miaka 11 ,amewataka viongozi wakisisa Kwale kuiga mfano wa shirika la samba sports na kupiga jeki juhudi za vijana za kujiinua kimaisha badala ya kuwatumia kuzua vurugu wakati wa kampeni za kisiasa ,ili wafanikishe malengo yao binafsi .
“ Viongozi wa kisiasa wanatupa kipau mbele tu wakati wa kampeni za kisiasa kwa sababu wanatuona wanyonge , hii samba sports ni tunu Mungu ameileta na ni sharti viongozi washirikiane nao katika juhudi za kuafikia ndoto zetu ili tunaishi katika mazingira salama ,” Asema bw. Abdallah
Kwa upande wake Abdallah Idd Ali wa Atlantico FC ,amesifia mradi wa kujenga amani ,huku akiwataka vijana wenza kujinasua katika visa vya uhalifu na badala yake wachangamkie shughuli zinazowapatia fedha za halali ama wajiunge na vilabu vya soka .
“ Natoa wito kwa vijana wenzangu kudumisha amani na usalama ,kwani hakuna maendeleo yanaeza fanyika bila amani na usalama ,”Asisitiza bw.Ali
Athman Hamisi Wari kutoka kikundi cha Fikra Youth Group kutoka Kiteje ni kati makundi mengi yaliyofaidika na pembejeo za kibiashara kutoka kwa shirika la samba sports youth ajenda ,akiema kwamba pembejeo hio itawasaidia kuanzisha miradi itakayobuni ajira binafsi kwa vijana .
“ Sababu kuu inayowafanya vijana kuketi maskani na kujiingiza katika magenge ni ukosefu wa shughuli za kufanya , jambo lolote likitokea mitaani la kihalifu washukiwa ni wale vijana wanaoketi maskani , kwa sasa pembejeo kama hizi ambazo tumezipataka kutoka kwa sambasports youth agenda zitatusaidia pakubwa kupunguza uhalifu , kama kikundi chetu ni cha kupangilia sherehe na tumepata viti ,sasa shughuli yoyote tukialikwa tutawahusisha vijana hata wale wa maskani na zile shughuli mbovu wanazozifanya wataziacha,”Asema bw.Wari .
Mbali na kuwanasua vijana kutoka kwa magenge ya uhalifu ,sambasports imekua ikishirikiana na wadau mbalimbali kukuza vipaji vya vijana wakike na wale wakiume kufikia ngazi za juu zaidi katika Nyanja ya soka , Binti Omar Juma Changu ni kati ya marefa 25 kata ya Waa wauliofuzu kupitia mradi wa SHIFT uliofadhiliwa na Basetitanium.
“ Nafurahi kufuzu kama refa , tulipata mafunzo ya urefa tukiwa wasichana 6 na wavulana 19 ,nashukru sana kwa kufikia hatua hii , kazi ya urefa sio ya wanaume pekee hata wasichana wanaezafanya , naamini huu ndio mwanzo wakufikia ndoto zangu katika soka,”Asema bi.Changu .
Mwanadada Asha Njama almaarufu Boss lady wa Wellers FC ni kati ya makocha 30 waliofuzu kupitia mradi wa SHIFT uliotekelezwa na shirika la samba sports youth agenda
“ Najivunia kuwa kocha wakike ,ni nafasi niliyoitamani kwa muda mrefu sana na nashkru kuifikia ,katika mazingira ya mila na tamaduni yetu sio rahisi kwa mwanadada kuwa katika nafasi hii ama kucheza soka lakini mimi nimeweza , mimi nilipenda soka nikiwa na umri mdogo na leo hii nafurahi sana maana ndoto yangu yaendelea kutimia ,”Asema bi.Njama.
Abigael Ndizi ni kati ya wanadada wanane waliofuzu katika kitengo cha waamuzi wa ndani katika awamu ya pili ya mpango huo ,akisema kuwa ndoto yake nikuchezesha timu za kimataifa.
“ Mimi niliamua kuwa muamuzi wa kati kati kwa sababu nataka kubadilisha mtazamo wa mtoto wakike katika jamii ,ikiwa wanaume wanaeza ,msichana pia anaweza ,hakuna kitu ambacho hakiezekani ,”Asema bi.Ndizi .
Mwakilishi wa akinamama kaunti ya Kwale Fatuma Masito akiahidi kushirikiana na shirika la sambasports youth agenda katika maswala ya kuimarisha maadili ya vijana ili kuona kuwa amani inashamiri na jamii zinaishi katika mazingira salama .
Hata hivyo idara ya usalama kwale imekuwa ikiendeleza doria za mara kwa mara katika maeneo yaliyo na michipuko ya magenge ya kihalifu ili kuimarisha usalama na kuona kuwa washukiwa wanakabiliwa kisheria , huku ikitangaza kuthibiti michezo ya soka kwa kisingio kuwa imekuwa maficho ya wahalifu ,,je kuthibiti soka inaezakuwa suluhu la kudumu la uhalifu ama kuzidisha michipuko Zaidi ?
Imekuwa mtindo sasa wa wanasiasa wengi kutumia soka kama chombo cha kujipigia debe na kisha kuwatelekeza pindi wanapoingia mamlakani ,wasifahamu kuwa soka ni chombo thabiti cha kuimarisha maadili ya vijana na kuhakikisha jamii salama .
Soka au kandakanda kama inavyojulikana katika sehemu nyingi za dunia imetawala katika bara la afrika ,umaarufu ulioenea katika bara zima sio kwa bahati mbaya .
Uzuri wa soka upo katika urahisi na upatikanaji wake ,ni mchezo unaohitaji vifaa kidogo –mpira na kitu cha kuashiria lango ,hata miamba michache tu .
Urahisi huu unamaanisha kuwa soka inaweza kuchezwa popote barani afrika .
Comments
Post a Comment