Watoto wanaougua magonjwa ya moyo ya kuzaliwa wana matumaini ya kuishi hadi uzeeni endapo watagundulika na kupatiwa matibabu ya haraka.
Taarifa yake : Caroline Katana
Lucy Kadzo katika kijiji cha Menza Mwenye ,Lungalunga kaunti ya Kwale ni kati ya watoto waliopona ugonjwa wa moyo wa kuzaliwa (congenital heart disease ) baada ya kugunduliwa na kupata tiba ya haraka katika hospitali ya rufaa ya Msambweni .
Mtoto Lucy mwenye umri wa miaka 8 , grade ya pili ,aligundulika akiwa na umri wa mwaka mmoja katika hospitali ya Lungalunga kabla ya kutumwa katika hospitali ya rufaa ya Mswambweni kwa uchunguzi zaidi.
Joyce Dama Tsuma mama wa watoto wawili , anasema kuwa alianza safari ya matibabu ya kifungua mimba wake Lucy mwaka 2017 , japo kueleza safari ya kutafuta matibabu ya mwanawe kukosa matumaini kufuatia gharama za juu za matibabu ya moyo ,mwanawe Lucy sasa ni buheri wa afya baada ya wahisani kujitokeza na kufadhili matibabu yake .
“ Nilipopata majibu kuwa moyo wa mtoto wangu umefura ,nilikata tamaa ya kuona mwanangu akiishi kwa mara nyengine ,watu wengi walinikatisha tamaa kwa kusema nchini kenya hakuna matibabu ya moyo hadi ,taifa la India na gharama zake ni ghali mno ,japo kunao walionitia moyo ,Imani yangu ilishuka sana na nikajua ningempoteza mwanangu muda wowote ,” Asema bi Tsuma .
Hata licha ya baadhi ya familia kuwa na mtazamo tofauti dhidi ya watoto wanaozaliwa na magonjwa yasiyoambukiza ,bi Tsumi akiri familia ya mumewe kusimama pamoja nae katika safari hio ya kusaka matibabu ya mwanawe .
“ Magonjwa haya yamekuwa yakionekana kama laana ama kuhushishwa na ushirikina ,na awali watoto waliokuwa na magonjwa haya walikuwa wakiuwawa ama mama kufukuzwa katika boma ,lakini kwangu hali ilikuwa tofauti kwani familia ilinitia moyo hadi kufikia mwisho wa safari hii ,”Asema bi Tsuma .
Katika kambi ya uchunguzi wa moyo kwa watoto iliyifanyika katika hospitali ya rufaa ya Msambweni ,tarehe 7, Novemba 2024 ,bi Tsuma anaonekana akiwa mwingi wa furaha baada ya wataalam wa uchunguzi wa magonjwa ya moyo kwa watoto kutoka hospitali ya Coast General kumthibitishia kupona kikamilifu kwa mwanawe Lucy Kadzo , Lucy akionekana kuwa buheri wa afya kwa mara nyingine baada ya safari ya miaka 7.
Bi. Tsuma sasa ameishauri jamii kukomesha unyanyapaa ,dhana potofu dhidi ya magonjwa yasiyoambukiza na badala yake kuitaka jamii kuchukua hatua za haraka za kutafuta matibabu pindi watoto wao wanapopatikana na magonjwa yasiyoambukiza .
Takwimu mbalimbali zikiwemo za Shirika la Afya Duniani WHO zinaonesha kuwa watoto wengi hufariki kabla ya mwaka mmoja kwa ugonjwa wa moyo bila kugundulika na kupatiwa matibabu ya haraka .
Tunaelezwa kuwa matatizo ya kuzaliwa ya moyo hutokea katika watoto 4 hadi 9 katika kila vichanga 1,000 vinavyozaliwa , mataifa ya uchumi wa chini na yale yanayo endelea kukua kiuchumi yakionenekana kuathirika hata Zaidi.
Daktari muuguzi katika wodi ya watoto katika hospitali ya rufaa ya Msambweni Dr .Saumu Koja aliyeandaa kambi ya uchunguzi wa magonjwa ya moyo kwa watoto amethibisha zaidi ya asilimia 50 ya watoto Kwale kuugua magonjwa ya moyo mwaka huu .
“ Tumepanga hii kambi ili watoto waweze kupata huduma ya uchunguzi bila malipo ,mwaka huu pekee tumeona Zaidi ya watoto asilimia 50 wakiwa na matatizo ya moyo na wazazi hao hawana uwezo wa kusimamia gharama za matibabu ,” Asema Daktari . Saumu .
Akidokeza kuwa katika kambi hio pia wazazi wanaelimishwa uhumuhimu wa kuzingatia lishe bora na kuepuka msongo wa mawazo wanapokuwa wajawazito ili kueka magonjwa yasiyoambukiza kwa watoto wao .
Kadhalka ameeleza kutoridhishwa kwake na jinsi mpango wa serikali wa bima ya afya SHA kutenga asilimia ndogo sana ya fedha ya kusimamia magonjwa yasiyoambukiza licha ya kuwa ya gharama ya juu mno ya matibabu .
“ Mpango wa serikali wa fya ya jamii SHA haujamsaidia mkenya anayeishi na magonjwa yasiyo ya kuambikiza kwa sababu mgao wake ni mchache mno ,ikilinganishwa na gharama za juu za matibabu ya magonjwa hayo , uchunguzi wa moyo pekee unagharim hadi shilingi elfu 10 ,fedha ambazo jamii nyingi zinashindwa kupata ,” Asema daktari saumu.
Barani Afrika magongwa ya moyo kwa watoto yakisalia kuwa mzigo mkubwa mno baada ya wizara ya afya kutia nguvu zaidi ya kupambana na magonjwa kama vile Malaria ,Kuhara na Pneumonia miongoni mwa watoto huku magonjwa ya moyo ya kuzaliwa miongoni mwa watoto yakisahaulika ,mzigo wa magonjwa hayo ukionekana kuongezeka siku baada ya siku .
Serikali ya Kenya bado haijaekeza kikamilifi katika juhudi za kupambana na magonjwa yasiyoambukiza kwa watoto kama vile maradhi yanayoambukiza licha ya magonjwa hayo kuwa tishio kubwa la afya ya watoto katika siku zao za usoni .
Uhaba wa vituo na wataalam wakutibu magonjwa ya moyo ikiwa changamoto kuu katika juhudi za kupambana na magonjwa hayo .
Taifa la Kenya vituo vine pekee vya kushughulikia magonjwa ya moyo katika kaunti ya Nairobi ,Mombasa ,Kisumu na Eldoret ,vituo viwili pekee vikitoa huduma kamili ya magonjwa hayo ,vituo hivyo vikitajwa kushindwa kuhimili idadi kubwa ya wagonjwa wanaohitaji huduma
Kituo cha kushughulikia magonjwa ya moyo katika hospitali ya Coast General kilichozinduliwa mwaka wa 2019 ni kati ya vituo vine vya humu nchini na hadi kufikia sasa kimeshughulikia , watoto 1100 na watoto 600 walipatikana na magonjwa ya moyo .
“ Asilimia 75 ya watoto wanaugua magonjwa ya moyo ya kuzaliwa (Congenital heart disease) huku asilimia 10 ikiwa Rheumatic heart disease ,asilimia 10 Dilated cardiomyopathy na asilimia 5 ikiwa ya aina mbalimbali ya magonjwa ya moyo kwa watoto ,” Asema mtaalam wa magonjwa ya moyo katika hospitali ya Coast General Zainabu mubarak .
Daktari zainabu akiafiki magonjwa ya moyo miongoni mwa watoto kuongezeka kwa kiwango cha kutisha .
“ Wazazi wengi wanajifungua watoto wenye magonjwa ya moyo lakini bado hawana ufahamu na Afrika nzima hakuna takwimu kamili za watoto wanaougua moyo kwa sababu magonjwa yasiambukiza kwa watoto yamesahaulika ,serikali zimepea kipao mbele magonjwa ya watu wazima pekee , ukiangalia hata wataalam wa moyo ni wachache ,vituo pia ni kidogo afrika nzima ,kwa sababu maswala ya watoto hayashughulikiwi ,”asema daktari Mubarak .
Daktari zainabu akisema kuwa watoto hao 200 wenye magonjwa ya moyo ya kuzaliwa na Rheumatic heart disease walishughulikiwa kupitia kufunga mashimo ama oparesheni ya kufungua mishipa iliyofunga katika kituo hicho cha Coast General .
Daktari Zainabu akisema kuwa kliniki 16 za uchunguzi wa moyo walizofanya katika kaunti 8 za humu nchini zimeonyesha kuwa kaunti ya Garisa iko na rekodi ya juu ya visa vya watoto kuugua magonjwa ya moyo .
“magonjwa haya yako sana katika sehemu ambazo kuna ugumu wa kufikia vituo vya afya ,kaunti ya Garisa ndio iko na rekodi ya juu ya asilimia 48 ,eneo la kinango kaunti yak wale asilimia 42 ,Mandera asilimia 44 miongoni mwa sehemu zengine za nchi ,” asema daktari Mubarak .
Daktari zainabu akieleza kuwa ili kuwapunguzia gharama za matibabu wazazi walio na watoto wenye magonjwa ya moyo , amekuwa akitafuta wahisani kutoka mataifa ya nje ambao hutoa huduma za matibabu ya moyo bila malipo .
“ Watoto wengi wenye haya magonjwa wanatoka katika familia zisizojiweza ,ndio maana tunajaribu kuwasaidia kupitia kwa marafiki wetu ambao huwapatia huduma bila malipo ,tuko na vituo binafsi vya kutibu magonjwa ya moyo kwa watoto lakini ni ghali mno ,ili kupata huduma mzazi ni sharti alipe Zaidi ya milioni moja ,ambapo jamii yetu haiwezi ,” Asema daktari zainabu.
Changamoto zilizozingira juhudi za kukabiliana na magonjwa ya moyo kwa watoto :
-uhaba wa vituo na wataalam - uhaba wa fedha kutoka kwa serikali -umaskini -unyanyapaa -ukosefu wa hamasa kwa jamii dhidi ya magonjwa yasiyoambukiza -kuvunjika kwa familia -mila na tamaduni potofu - vifo -ukosefu wa nambari ya mawasiliano - ukosefu wa lishe bora na msongo wa mawazo kwa akinamama wajawazito .
Mapendekezo kwa serikali na jamii
Mtaalam huyo ameitaka serikali ya kitaifa na zile kaunti kuhakikisha zinaekeza zaidi katika magonjwa yasiyoambukiza kwa watoto , serikali kupunguza gharama za matibabu ,wazazi kuzingatia lishe bora na kuepuka msongo wa mawazo wanapokua wajawazito , jamii kukomesha unyanyapaa ,mila na tamaduni potofu dhidi ya magonjwa yasiyoambukiza kwa watoto ,akinamama kuwapeleka watoto kliniki kwa wakati ,kujengwa uwezo kwa wataalam wa magonjwa ya moyo nchini .
Taifa la Kenya linaendelea kushuhudia mzigo mkubwa wa kutibu magonjwa yasiyo ya kuambukiza ,hususan magonjwa ya moyo ya kuzaliwa na watoto wengi wanazidi kuteseka kimya kimya na kufariki majumbani mwao baada ya wazazi wao kushindwa kugharamia matibabu .
Baraza linaloshughulikia magonjwa yasiyoambukiza nchini ( NCD Alliance Kenya ) linatambua juhudi za serikali za kuimarisha huduma za afya kupitia mpango wa afya ya jamii SHA , hata hivyo limeitaka serikali kuzingatia changamoto na mapungufu ambayo yamejitokeza katika mpango huo na kusababisha kilio cha umma kwa kuzindisha hali ngumu ya watu wenye magonjwa yasiyo ya kuambukiza kupata huduma za afya na kuzidi kuchangia matatizo ya afya ya akili miongoni mwa jamii .

Comments
Post a Comment