HAJA YA WAKULIMA KUFAHAMU AFYA YA MCHANGA WA MASHAMBA YAO.
Taarifa yake : Caroline Katana
Shirika la utafiti wa kilimo na mifugo nchini KALRO linaendeleza zoezi la kukusanya sampuli ya mchanga katika kaunti 45 za humu nchini ili kutoa mapendekezo kwa serikali kuhusiana na swala la utumizi wa mbolea katika kila kaunti , baada ya zoezi la utafiti katika maabara kukamilika .
Malengo ya utafiti huo ni kuhakikisha wakulima wanajua afya ya mchanga wao na kutumia mbolea iliyo sahihi katika mashamba yao ili kuinua viwango vya uzalishaji na kupunguza gharama za ununuzi wa chakula kutoka mataifa ya nje .
Zoezi hilo lililotia nanga mwezi huu na kutarajiwa kukamilika kati kati ya mwezi Machi ,linafadhiliwa na serikali ya Kenya na benki kuu ya dunia .
Taifa la kenya kwa sasa likiwa limepunguza kwa asilimia 30 uagizaji mahindi kutoka mataifa ya nje tangu serikali kuanzisha mpango wa mbolea ya bei nafuu kwa wakulima.
Licha ya mpango huo wa mbolea ya bei nafuu kutekelezwa na serikali wakulima hawana habari sahihi za aina ya mbolea wanayofaa kutumia.
Mwanasayansi mkuu wa utafiti, katika kitengo cha mazingira ,hali ya mchanga na mali asili ,katika shirika la KALRO Dr.Michael Okoti ,aliyekuwa akizungumza na waandishi habari katika afisi za KALRO Matuga ,kaunti ya Kwale amesema kuwa mkulima anafaa kujua afya ya mchanga kila baada ya miaka mitatu .
“ Kisayansi mkulima anafaa kujua hali ya mchanga wa shamba lake baada ya kuutumia ,kwa miaka mitatu , ambapo mkulima atalipa ada ya shilingi 900 ,baada ya zoezi hilo linalogharamiwa na serikali kukamilika ,” Asema Dr.Okoti .
Aidha mwanasayansi huyo amehoji kuwa kaunti ya Kwale iko na vituo 1,300 vya kuchukua sampuli za mchanga ambavyo zimetengwa kwa njia za kiutaalam na vitawakilisha kaunti nzima ya Kwale wakati majibu yatakapotolewa .
“ Utafiti wa mchanga Kwale utafanyika katika kila wadi na wakulima watajulishwa matokeo ,ili wajue aina ya mbolea ya kutumia katika mashamba yao ili kuboresha mazao ,” Asema Dr.Okoti .
Kadhalka amedokeza kuwa KALRO kwa ushirikiano na wadau wengine wako mbioni kuunda mfumo wakidijitali utakaowawezesha wakulima kujua mbolea hitajika kwa mashamba yao kabla ya mwaka huu kukamilika .
Msimamizi wa kituo cha KALRO Matuga Dr. Finyange Pole ,amesema kuwa wakulima wengi hususan eneo la pwani wamekuwa wakilima bila kutumia pembejeo kama mbolea hatua inayowapelekea kupata mazao duni kila msimu wa mavuno .
“Wakulima wanapaswa kujua kuwa kila wakati wakilima na kuvuna wanapunguza rotuba kwenye mchanga ,hivyo wakati umefika sasa wametumie mbolea iliyo sahihi kwa mimea yao,” Asema Dr. Pole .
Wakati uo huo amewataka wakulima kukomesha mila na itikadi Potofu dhidi ya utumizi wa mbolea .
“ Hapa Kwale kuna wakulima hata ukiwapatia mbolea bure hawataitumia ,wako na dhana potofu kuwa mbolea inaharibu mchanga ,jambo ambalo sio la kweli ,” Asema Dr.Pole
Ametoa changamoto kwa wakulima eneo la Kinango na wadi ya Dzombo huko Lungalunga kukomesha itikadi hizo kwa manufaa yao .
“Wakati mwingine hata tukienda kuchukua sampuli za mchanga wengine hata hutufukuza ,wakidhania kuwa tunaenda kuuza mchanga ama kuupeleka kwa washirikina ili kuwaharibia mazao yao ,na sisi malengo yetu ni kuhakikisha wanatumia mbolea iliyo sahihi na kuongeza mazao yao ,” Asema Dr. Pole .
Wakati uo huo ameeleza kuwa licha ya eneo la Pwani kuwa na uwezo wakujilisha na kulisha kaunti zengine ,bado eneo hilo linauzalishaji wa chakula wa asilimia 30 pekee ,likisalia kutegemea chakula kutoka kaunti zengine za humu nchini .
“ Sekta ya kilimo ili gatuliwa na ni jukumu la kila kaunti walipe kipaombele swala za uzalishaji wa chakula ,na tukilisha watu wetu vizuri hakutakuwa na haja ya kujenga hospitali na zahanati nyingi mana magonjwa mengi haswa yale yasiyoambukiwa yanakuja kwa kukosa lishe bora ,”Asisitiza Dr. Pole.
Beauty Tatu Matata kutoka kijiji cha Tumbula wadi ya Waa –ng’ombeni ni mkulima mfugaji anayeendeleza kilimo biashara ambaye amehiari kufanyiwa upimaji wa mchanga wa shamba lake .
“ Ningependa sana kupimiwa huu mchanga ili niweze kujua aina ya mbolea ninayofaa kutumia ili niweze kupata mazao mengi Zaidi yatakayo nipa faida kubwa ,”Asema bi .Matata .
Aidha ameeleza kuwa mabadiliko ya tabia nchi ,uvamizi wa wadudu na wanyamapori ni baadhi ya changamoto sugu zinazolemaza kilimo chake .
“ Ukilima mahindi inakulazimu ueke ulinzi hadi siku ya kuvuna ,huku kuna uvamizi wa nguruwe, ndege na manyani ila kuutaja uvamizi wa wadudu kwenye mimea kumnyima lepe la usingizi ,” Asema bi .Matata .
Bi .Matata akisema kuwa ndoto yake ni kuwa mkulima wakimataifa ,akiitaka serikali ya Kwale na wadau mbali mbali wa kilimo kujitokeza na kusaidia wakulima kukabiliana na changamoto hizo.
“ Nilipenda kilimo tangu nikiwa mtoto mdogo na ningependa kudumu katika kilimo ,maono yangu ni kuzalisha chakula Zaidi cha matumizi ya nyumbani na kibiashara ,maana hii ni ajira binafsi,”Aeleza bi Matata .
Ali Omar Siri ni mkulima mfugaji katika eneo la Patanani ambae pia amelipokea vyema zoezi la upimaji wa mchanga unaoendelezwa na shirika la KALRO .
“ Zoezi hili ni muhimu sana, kwa maana utajua mapungufu yaliyopo katika mchanga na itakuwa rahisi kujua aina ya mbolea sahihi yakutumia ili niweze kupata mazao bora Zaidi , mchanga huu uko na madini tofauti tofauti kwa hio baada ya utafiti nitajulishwa ni kipi cha kufanya ili uzalishaji uboreke ,” Asema bw.Siri .
Bw. Siri amewataka wakulima kaunti ya Kwale kukumbatia zoezi hilo linalolenga kuboresha mazao na kuhakikisha usalama wa chakula katika siku za usoni ,kwani kwa miongo mingi kaunti ya Kwale imekuwa ikikumbwa na makali ya njaa.
Comments
Post a Comment