Mapungufu katika mswada wa hazina ya mikopo ya biashara ya Kwale mwaka 2024
Caroline Katana
Mswada wa hazina ya mikopo ya biashara wa kaunti ya Kwale mwaka 2024 ( kwale county biashara revolving fund bill 2024 ) umezingirwa na mapungufu msingi yanayohitaji kurekebishwa kabla ya kupitishwa na kuwa sheria, ili uwafaidi walengwa .
Haya yameibuka katika mkao wa kuuchanganua mswada huo ,ulioleta pamoja mashirika mbalimbali ya kijamii chini ya muungano wa mashirika wa Kwale Community of Practice ,huko Diani kaunti ya Kwale .
Kwale community of Practice , inachanganua mswada huo wa biashara 2024 na kunakili mapungufu yaliyomo kabla ya kuandika Memo ya mapendekezo ya marekebisho katika wizara husika .
Mswada huo utakapokuwa sheria ,utaondoa miswada miwili , ule wa fedha za mikopo za mzunguko (revolving fund) na ule wa vijana ,akinamama na watu wanaoishi na uwezo maalum .
Licha ya mswada huo kukosa kujumuisha sekta nzima ya biashara kaunti ya K wale na kuangazia utoaji mikopo kwa wenye kampuni ,utakapokuwa sheria utatengewa shilingi Bilioni Moja .
Mchanganuzi wa mswala ya bajeti na uongozi kaunti ya Kwale Jalim Mohamed Ibrahim amesema kuwa mojawapo wa mapengo yaliyoko katika mswada huo ni kukosa sera ya mwongozo .
“ Mswada huu kabla haujapitishwa ama kuzungumziwa unafaa uelezee mapungufu yaliyoko katika miswada hio miwili inayofaa kuondolewa , ndio baadae wakaazi waelezewe kuhusiana na mswada huu mpya ,lakini mambo haya hayajaekwa bayana ,” Asema bw Jalim .
Bw. Jalim akishangazwa na jinsi miswada kaunti ya Kwale inavyoonekana kuwa na usawa hususan katika mfumo wa uchaguzi wa kamati ama bodi simamizi za sheria .
“Tukiangalia mfumo wa uteuzi wa kamati simamizi katika mswada huu ,ni sawasawa na mswada uliopitishwa wa fedha wa Pubic Finance Management Act (PFM ) 2012 ,kipengee 137 kinazungumzia kwamba mwenyekiti wa bodi ya CBEF anachaguliwa na gavana ,na kufikia sasa miswada yote inaoonekana kufuata mtindo huo ,na hili mara nyingi huwa linaleta siasa ndani yake ,ili mswada umsaidie mwananchi ,siasa inafaa iondoke ,ikiwa siasa itaekwa mbele basi huu mswada hautamsaidia mkaazi ,”Asema bw.Jalim .
“Sheria ya katiba kipengee 38 kinazungumzia haki za siasa ,ambapo kila mtu ana malengo yake kwenye siasa ,hivyo endapo mkaazi atafeli kumuunga mkono gavana huenda akakosa mambo muhimu ,endapo mwenyekiti wa kamati simamizi ya kaunti atachaguliwa na gavana sauti yote ya utoaji mikopo itakuwa ya kisiasa ,”
Swala la waziri wa biashara , viwanda na vyama vya ushirika kuwachagua wawakilishi wa jamii katika mswada huo likionekana kuwa tete .
“ Katika mswda huo , Vijana ,akinamama na watu wanaoishi na uwezo maalum wamependekezwa kuchaguliwa na waziri ,mbona wasipewe nafasi ya kuchaguana wenyewe kwa wenyewe kwa sababu wanajamii wanajuana ,hii inamaanisha kuwa kutakuwa na ubaguzi ,kwani waziri atachagua watu anaowafahamu na kama huna ukaribu nae inamaana hutaeza kupata hio nafasi ya kuwakilisha jamii,” Aeleza bw.Jalim .
Akigusia swala la kamati katika kila wadi za kaunti hio bw Jalim amesema kuwa hatua hio inalenga kumkandamiza mlipa ushuru .
“ Kwale iko na wadi ishirini hivyo endapo kamati hizi zitachaguliwa, itakuwa mzigo kwa mlipa ushuru kwani itapandisha bili ya ulipaji fedha ( wage bill ) iwe mishara ama marupurupu , na utumizi wa fedha ukipanda Zaidi itamaanisha hata pesa za kutekeleza miradi ya maendeleo itapungua ,lengo la ugatuzi nikuleta rasilimali mashinani ili wananchi wapate kufaidika na maendeleo ,iwapo pesa hizi zitaenda kwa mifuko ya watu inamaana baadhi ya miradi itakosa kutekelezwa ,”
“ Mwaka wakifedha 2023/2024 kaunti ya Kwale ilipata mgao mkubwa Zaidi wa bilioni 11.2 ,bilioni moja ikitolewa sababu ya mikopo peke yake na hakuna uhakika kuwa pesa hii itarudishwa ,kumaanisha kutakuwa na pengo kwa ile pesa yetu , kimimi nasema hio bilioni moja isitolewe yote ikiwezekana iekwe milioni 250 ,kwa sababu ndio mwanzo wa sheria hii ,tukipata kuwa watu wanakumbatia tamaduni ya ulipaji basi iongezwe poleple kama vile mfuko wa basari ulivyoanza,” Apendekeza bw.Jalim
Mwakilishi wa Diani CP Caregivers Organization ambae pia ni kiongozi wa kitengo cha afya katika muungano wa Kwale Community of Practice Winnie Juma amesema kuwa uchanganuzi wa mswada huo umeleta uelewa miongoni mwa wanachama wa mashirika hayo ambayo ndio kiungo muhimu katika maswala ya kuelimisha jamii .
“Tumeweza kuelewa huo mswada wote kutoka kwa uteuzi wa kamati na majukumu yao kwa jamii ,sisi ni wawakilishi wa jamii na hii elimu tumepata leo tutaweza kuipeleka kwa mashinani kabla ya mswada huu kuanza kutolewa maoni na wakaazi kuanzia tarehe 10 ya mwezi huu , ili kuhakikisha jamii inatoa mapendekezo sahihi kuhusu mswada huu ,”Asema bi Winnie .
Bi .winnie akisema kuwa endapo mapungufu yaliyopo katika mswada huo yatajazwa basi walengwa watafaidika kikamilifu .
“Katika huu uteuzi wa kamati nzima ya kaunti , ni lazima iwe wazi jinsi hii kamati itawezaje kuwakilisha wakaazi wote wa Kwale bila ubaguzi ,ukiangalia maswala ya kazi ,vijana wengi na akinamama hawana ajira ,mswada huu ukipitishwa unafaa uzingatie jinsi wakaazi watakavyowakilishwa katika hii sheria ,”Aeleza bi Winnie
Wawili hao wametoa changamoto kwa watunga sheria kaunti ya Kwale kuhakikisha wanafanya utafiti ili wajua matakwa ya wananchi .
“ Inafaa waangazie aina za biashara za wananchi ,mswada huu unazungumzia maswala ya kusajili kampuni ,je wakaazi wengi wa Kwale wanakampuni , jibu ni hakuna ,je mtu binafsi anaweza faidika na hii pesa, kwa mfano mfanyibiashara akipewa shilingi elfu 50 haiwezi kumsaidia ,kabla watengeze miswada inafaa waangalie hali halisi ya wananchi kule mashinani ,miswada inafaa iwe na matakwa ya wanachi ,iwapo miswada itatengezwa pasi na kuzingatia changamoto za wakaazi basi miswada hio haiwasaidii wakaazi ,”
Hata hivyo wameitaka jamii kujitokeza kwa wingi na kushiriki katika vikao vya utoaji maoni ili kuzungumza kauli zao kwani wako na fursa ya kuukubali ama kuukataa .
“ Tunawaomba wakaazi wajitokeze kwa wingi na waulize maswali kuhusu huu mswada na pia waulize takwim ya kuonyesha ni watu wangapi walifaidika na ile miswada iliyopita ,”
Vikao vya utoaji maoni kuhusu mswada huu vitaanza rasmi tarehe 10 hadi tarehe 14 mwezi February .
Comments
Post a Comment